Dodoma. Rais mstaafu, Benjamin
Mkapa na mawaziri wakuu wastaafu, Frederick Sumaye na Cleopa Msuya, jana
hawakuhudhuria uzinduzi wa Bunge la Maalumu la Katiba kama ambavyo
ilitangazwa na Katibu wa Bunge la Katiba.
Katibu wa Bunge la Katiba Yahaya Khamis Hamad,
alitangaza juzi kuwa viongozi wote wastaafu, wamealikwa katika shughuli
za uzinduzi huo wa kihistoria wa Bunge hilo.
Wengine ambao hawakuhudhuria ni Rais mstaafu wa
Zanzibar Dk Salmin Amour na Waziri mkuu mstaafu, Dk Salim Ahmed Salim na
mke wa Rais wa kwanza wa Zanzibar, Fatma Karume.
Viongozi walio madarakani waliohudhuria uzinduzi
huo ni Rais wa Zanzibar Dk Ali Mohammed Shein aliyefika saa 9:23, Makamu
wa kwanza wa Rais Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad, Makamu wa Rais na
Dk Mohamed Gharib Bilal aliyewasili Viwanja vya Bunge saa 9:28 alasiri.
Rais Jakaya Kikwete alifika katika viwanja hivyo
saa 9:42 ambapo alipokewa na Mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba,
Samuel Sitta na baadaye kukagua gwaride lililoandaliwa maalumu kwa ajili
ya uzinduzi wa Bunge la Katiba.
Baadhi ya viongozi wakuu wastaafu waliohudhuria ni
Ali Hassan Mwinyi, aliyewasili Viwanja vya Bunge saa 9:10 na Rais
mstaafu wa Zanzibar, Aman Karume, aliyewasili saa 9:06.
Wengine ni Waziri Mkuu mstaafu John Malecela,
ambaye aliwasili Viwanja vya Bunge saa 9:13, mke wa Baba wa Taifa Maria
Nyerere na Spika wa Bunge mstaafu Pius Msekwa.
Pia alikuwapo mke wa Rais, Salma Kikwete, mke wa
Makamu wa Rais, Asha Bilal, mke wa Rais wa Zanzibar, Mwamwema Shein na
mke wa Waziri Mkuu Mizengo Pinda, Tunu Pinda.
Katiba inayotumika sasa ya mwaka 1977 imefanyiwa
marekebisho mara 14. Bunge hilo la Katiba linatarajiwa kuanza kazi zake
Jumatatu ijayo.
CHANZO Mwanachi
CHANZO Mwanachi
0 maoni:
Chapisha Maoni